Featured

MWONGOZO WA KULEA VIFARANGA


Kwa kawaida au katika hali halisi, kazi ya kulea vifaranga hufanywa kuku mwenyewe. Hivyo ili kulea vifaranga, mfugaji ni lazima aige kuku anavyofanya. Ikumbukwe kuwa vifaranga husumbuliwa zaidi na hali mbaya ya hewa, magonjwa mbalimbali, kukosa chakula kisichofaa na kukosa uangalizi wa karibu. Ni lazima vifaranga waangaliwe kwa kuwapatia nyumba yenye joto, chakula kinachofaa na maji safi , kuwakinga dhidi ya magonjwa masumbufu kwenye eneo husika na kuwatibu wanapougua. Mfugaji anayefanikiwa ni yule anayelea vifaranga wenye afya nzuri ambao hatimaye hutoa mazao mengi yanayompa faida.
Wafugaji wengi vijijini wamezoea kumwachia mama kuku kufuga vifaranga wake kwa muda mrefu hadi wajitegemee. Njia hii humchelewesha kuku kurudia kutaga na hivyo kupata vifaranga wachache zaidi kwa mwaka. Lakini vifaranga vikiondolewa kwa kuku mapema, kama majuma matano hivi baada ya kuanguliwa, na wakatunzwa na mfugaji, kuku hutaga
mapema na idadi ya kuku kwa mfugaji huongezeka haraka ndani ya kipindi kifupi.
Mwongozo huu unaeleza jinsi ya kufuga vifaranga vizuri ili hatimaye mfugaji apate faida zaidi.

SEHEMU YA KWANZA

NYUMBA YA KULELEA VIFARANGA
Ukipenda kujenga nyumba ya vifaranga itafaa ufi kirie yafuatayo:-
a)    Nyumba ya vifaranga iwe karibu na nyumba yako mwenyewe ili uweze kuwakagua vifaranga wako mara kwa mara.
b)   Ijengwe hatua 20 au zaidi mbali na nyumba ya kuku wakubwa, hii ni kinga mojawapo ya kupunguza hatari ya maambukizi ya magonjwa.
c)     Nyumba ya vifaranga isiruhusu ubaridi au unyevu au wanyama waharibifu kuingia. Lakini nyumba iingize hewa na mwanga wa kutosha kila wakati.
d)    Nyumba iwe na eneo la kutosha ili vifaranga wapate nafasi ya kutembea kutafuta chakula na maji bila kubanana.
e)     Ijengwe kwenye sehemu isiyoelekea upepo unaotoka kwenye nyumba ya kuku wakubwa. Tahadhari hii husaidia vifaranga kuepukana na magonjwa yanayoenezwa na upepo.

Ukubwa wa Nyumba
http://ufugajimakini.blogspot.com/

Eneo: Vifaranga hawahitaji eneo kubwa katika muda wa majuma 4 ya kwanza. Nafasi inayohitajiwa kwa kukadiria ni meta za eneo 1 kwa kila vifaranga 16. Kwa mfano nyumba yenye Meta 10 za mraba inatosha kulea vifaranga 160 hadi umri wa majuma 4. Vipimo vya nyumba yenye eneo kama hili inaweza kuwa na hatua 5 kwa hatua 4 au hatua 3 kwa 3.25. Utajenga kutegemea na eneo ulilonalo. Baada ya majuma 4 ya umri ongeza nafasi na uwape vifaranga eneo la kuwatosha.

Sakafu: Sakafu nzuri katika nyumba ya vifaranga ikiwezekana inafaa ijengwe na simenti iliochanganywa na zege. Ili kupunguza gharama, unaweza kutumia vifaa vya ujenzi vinavyopatikana kirahisi katika eneo lako vitumikavyo kusiriba sakafu kama udongo wa kichuguu au unaweza kulainisha kinyesi cha ng’ombe kwa maji na kusiriba eneo lote la sakafu.

Ukuta: Ingefaa kuta za nyumba za kulea vifaranga za matofali, udongo, mabati au debe. Kuta za matofari na udongo zipigwe lipu ili kurahisisha usafishaji wa nyumba au umwagiaji wa dawa. Urefu wa kuta uwe tangu meta 1.8 – 2.4 (futi 6-8). Sehemu ya kutoka chini ya meta 0.9 – 1.2 (futi 3 – 4) izibwe na ukuta wa tofali au udongo na sehemu ya juu iliyobakia yenye meta 0.9 – 1.2 (futi) 3-4) ijengwe kwa wavu wa chuma au fito.

Mbao: Nguzo za miti au mbao zilowekwe dawa ya mbao kama vile “Dudu killer” au oili chafu ili kuzuia kuoza. Ukitumia miti ni vizuri uondoe magome ambayo yanaweza kuweka vimelea na wadudu.

Madirisha: Unaweza kutumia maboksi, mikeka ya magunia, mapazia ya magunia ni rahisi na yanaweza kuwekwa kwa kupigiliwa misumari kwenye dari na upande wa chini pazia ipigiliwe misumari kwenye ubao ili ininginie.Unaweza kukunja mapazia/magunia ili uingize hewa na mwanga wa kutosha katika nyumba ya vifaranga.

Paa: Mjengo wa paa uwe unaoweza kuwapatia vifaranga hewa ya kutosha hivyo paa liwe na tundu la kutoa nje hewa yenye joto. Kwa kadri utakavyoweza, unaweza kutumia madebe, mabati, makuti au nyasi n.k. kuezeka nyumba ya vifaranga. Sehemu ya paa ikianza kuvuja iezekwe bila kuchelewa.

Vyombo kwenye nyumba ya vifaranga
Kuna vyombo vingi pia njia nyingi zinazotumika katika kulea vifaranga kutegemeana na hali halisi ya mfugaji. Mfugaji kijijini anaweza kutumia vyombo vifuatavyo:

1. Vitalu
Vifaranga hutunzwa ndani ya kitalu kilichotengenezwa kwa mbao au karatasi
ngumu zinazotumika kujengea dari. Au katika mazingira ya kijijini unaweza
kutengeneza wigo wa mduara kwa magunia. Upana wake uwiane na wingi wa vifaranga ulionao na kina chake kama mita moja. Ukuta wake uwe na tabaka mbili za magunia hayo zilizoachana kwa nafasi ya inchi tatu au nne. Katikati ya nafasi hiyo jaza maranda ya mbao au pumba za mpunga. Tayari utakuwa umepata kitalu cha kulelea vifaranga. Ndani ya kitalu weka taa ya chemli(au balbu ya umeme kama umeme unapatikana) ya kutoa joto linalohitajika kwa vifaranga.

2. Taa ya chemli (taa ya mkono) au balbu ya umeme(kama umeme unapatikana)
Kutegemeana na hali ya hewa taa moja ya chemli inaweza kulea vifaranga 50 au zaidi. Hakikisha kuwa unayo akiba ya mafuta ya taa ya kutosha, vioo, utambi n.k. Taa moja hutumia debe moja la mafuta ya taa kwa muda wa siku 16 hadi 20. Unashauriwa uweke mafuta kwenye taa asubuhi na kukagua jioni kama yanatosha kwa sababu taa ikizimika usiku utapata hasara ya vifo kwa vifaranga kujikusanya na kukosa hewa .Weka mafuta ya kutosha lakini usijaze taa. Joto la taa za chemli hurekebisha kwa kupandisha au kushusha utambi pia kuongeza au kupunguza idadi ya taa.(tumia umeme kama unapaatikana mazingira unamoishi)

3. Jiko la Mkaa
Jiko la mkaa linaweza kutumika badala ya taa kwa ajili ya kuwapa vifaranga joto. Unapotumia jiko la mkaa ni hakikisha kwamba mkaa unaotumia hautoi moshi na chumba kinapitisha hewa safi na ya kutosha. Pia jiko liwekwe juu ya matofaili ili kuzuia vifaranga wasiliguse.

4. Mwamvuli
Mfugaji akimudu anaweza kutengeneza mwamvuli wa kuning’inia juu ya kitalu cha kulea vifaranga kwa kutumia makaratasi magumu ya “hardboard”. Mwamvuli unasaidia kupunguza upotevu wa joto na hivyo kupunguza matumizi ya mafuta ya taa. Kwenye mwamvuli wa duara toboa tundu moja ili kupitisha hewa yenye joto. Angalia mviringo wa mwamvuli wako uwiane na ukubwa wa kitalu chako. Ili kuwapa vifaranga uhuru wa kufuata au kuepuka joto. Ni lazima mwamvuli uwekwe juu ya matofali na kila juma inabidi uinuliwe juu kiasi cha cm 5 (inchi 2, kufuatana na hali ya hewa.

5. Vyombo vya chakula (Vihori)

http://ufugajimakini.blogspot.com/

Ili vifaranga wakue vizuri vyombo vya chakula lazima viwafae. Vipimo pamoja na idadi ya vyombo vya chakula ni vya muhimu viwatosheleze. Chombo chenye urefu wa (futi 3 x inch 3) kinatosha vifaranga 100. Ukitumia mbao kutengeneza vyombo vya chakula unashauriwa mbao ziwe unene wa cm 1/25 (inchi ½). Pia, unaweza kutumia sahani za kawaida unazotumia nyumbani kuwawekea vifaranga chakula.

6. Vyombo vya maji:
http://ufugajimakini.blogspot.com/

Chombo chochote chenye kina kifupi kinafaa kwa kuwayweshea kuku ila budi kiinuliwe ili vifaranga wasiweze kuingiza takataka za chini kwenye maji. Pia kama ni cha wazi maji yawekewe changarawe safi kabisa ili kuzuia vifaranga
wasiloane maji. Au tumia sahani na makopokama ifuatavyo. Toboa sentimita tatu kutoka kwenye mdomo wa kopo, jaza maji katika kopo halafu lifunike kwa sahani na ligeuze.

Subscribe to this Blog via Email :

1 comments:

Write comments
Unknown
AUTHOR
May 12, 2020 at 11:21 AM delete

Aisee Nimefurahi sana leo kufikia hii blog najifunza sana na nitatoa mrejesho na motisha kwa Wengine zaidi

Reply
avatar